WEMA, JOKATE WAMZOMEA DIAMOND!

KAMA mbwai na iwe mbwai tu! Hiyo ndiyo kauli pekee iliyoweza kuakisi kitendo cha warembo, Wema Sepetu ‘Madam’ na Jokate Mwegelo ‘Kidoti’ kuamua kumzomea zilipendwa wao, Nasibu Abdul ‘Diamond’ baada ya kuzidiwa tuzo na hasimu wake, Ali Kiba, Risasi Mchanganyiko lina full stori.
Jokate Mwegelo ‘Kidoti’ akicheka baada Ali Kiba kuchukua tuzo ya nne kwenye Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
ENEO LA TUKIO
Tukio hilo lililojidhihirisha laivu ni la chuki lilijiri wikiendi iliyopita kwenye Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam ambapo warembo hao walikuwa wamehudhuria kwenye sherehe za utoaji Tuzo za Kilimanjaro Music Award 2015, ambapo walishangilia kila Ali Kiba alipopata tuzo huku wakizomea pale Diamond alipopata.
Warembo, Wema Sepetu ‘Madam’ na Jokate Mwegelo ‘Kidoti’.
ZOMEA YANOGA
Warembo hao waliokuwa wamekaa sehemu tofauti ukumbini humo, kwa pamoja waliunganisha nguvu na kupata sapoti ya mashabiki wengine waliohudhuria hafla hiyo iliyomalizika kwa Ali Kiba kupata tuzo tano huku Diamond akiambulia mbili.
MCHANGANUO ULIVYO
Ali Kiba ambaye hakuwepo ukumbini na tuzo zake kupokelewa na mwakilishi, alijinyakulia tuzo za Mtumbuizaji Bora wa Mwaka, Wimbo Bora wa Mwaka (Mwana), Mtunzi Bora wa Mwaka (Bongo Fleva), Wimbo Bora wa Afro Pop (Mwana) na Mwimbaji Bora wa Kiume huku Diamond akitwaa za Wimbo Bora wa Zouk/Rhumba (Nitampata Wapi) na Video Bora ya Mwaka (MdogoMdogo).
Staa wa Bongo, Nasibu Abdul ‘Diamond’.
WAPENDA UBUYU WAHOJI
Kutokana na zomeazomea hiyo kuwa kubwa, waalikwa wanaojua kufuatilia mambo ya watu walianza kuhoji kulikoni Jokate na Wema waungane kumzomea Diamond wakati wao wenyewe hawapatani.
“Dah ama kweli mapenzi ya Kibongo si ya kuyatilia maanani, sitaki kuamini kama Wema huyu ni wa kuonekana beneti na Jokate wakati mwanzo walikuwa hawasalimiani, kingine kinachonishangaza leo Wema huyuhuyu aliwahi kutolewa nishai na Jokate ndani ya ukumbi huuhuu katika shoo ya Diamond are Forever eti leo ni marafiki wanakaa hadi wanapiga picha ya pamoja,” alisema mmoja wa mashabiki.
Wema Sepetu ‘Madam’.
‘AFTER PART’ SASA!
Kuonesha kuwa walidhamiria, baada ya shoo ya utoaji tuzo kumalizika, Wema alionekana akijipongeza na wenzake kwenye ukumbi maalumu ambao ulikuwa umeandaliwa (after party) akipiga ‘gambe’ na kucheza muziki kujipongeza sanjari na Jokate hadi kulipopambazuka.
DIAMOND ANASEMAJE?
Kutokana na hali hiyo kujionyesha waziwazi, siku iliyofuata, paparazi wetu alimtafuta Diamond ili kumsikia anazungumziaje suala la warembo hao kumzomea lakini hakutaka kuwazungumzia zaidi akafungukia tuzo hizo kwa jumla.
Staa wa Bongo, Ali Kiba.
“Kiukweli sina kinyongo, napenda kutoa pongezi kwa washiriki, washindi wote na waandaaji, bahati mbaya mimi sikuweza kuhudhuria maana nilikuwa Afrika Kusini kwenye hafla ya utambulisho wa wasanii waliochaguliwa kuwania Tuzo za MTV Base (MAMA’S), pamoja na kutokuwepo hapo naomba kuwafahamisha Watanzania kuwa nimefurahishwa na washindi wote na tuzo zote.
AJIPIGIA DEBE KIAINA
“Namshukuru Mungu pia kwangu mimi kuchaguliwa kwa mara nyingine katika kuwania Tuzo za MTV kwenye tuzo ya Msanii Bora wa kiume Afrika, Mtumbuizaji Bora wa Kiume Afrika na nyimbo Bora ya kushirikiana Afrika, naomba watu wote tuungane katika hili tena ili tuweze kupiga kura kwa wingi na kuleta heshima kwenye nchi yetu na Afrika kwa ujumla,” alisema Diamond.

Comments